Tuesday, June 15, 2010

DR.MANYAUNYAU


Wafurika polisi kuona wanaojiita Dk. Manyaunyau 2008-01-26 09:42:28 Na Idda Mushi, PST, Morogoro
Mamia ya wakazi wa Mkoa wa Morogoro jana walifurika katika kituo kikuu cha Polisi Mkoani Morogoro baada ya kukamatwa kwa waganga wa jadi wanaodaiwa kutapeli wananchi kwa kujiita `Dk. Manyaunyau`. Inaelezwa kuwa kukamatwa kwa watu kulitokana na mtu anayeaminika kuwa ndiye Dk. Manyaunyau halisi kufika Morogoro na kuwashitaki watuhumiwa kwa utapeli kuwa wanatumia jina lake vibaya na kwamba walikutwa wakiwa katika harakati za kuendelea `kutapeli`. Ilidaiwa kwamba `waganga` hao watatu waliokamatwa wamekuwa wakijikusanyia fedha katika mitaa mbalimbali wakidai kwamba wanataka kuisafisha dhidi ya uchawi. Kilichowavutia wengi kufika kituoni hapo ni kugundua kwamba kumbe waliokuwa wakijiita Dk. Manyaunyau siyo na kwamba mhusika amewasili kuwaumbua wale waliokuwa wakiwatapeli. Bw. Jongo Salum (27), mkazi wa Tabata Mawezi, Dar es Salaam, ambaye kwa madai yake ndiye Dk. Manyaunyau `halisi`, mwenye leseni ya tiba anayoilipia mamlaka ya mapato nchini (TRA), aliwaambia waandishi wa habari kwamba amesikitishwa na hatua ya watu hao kutumia jina lake katika tiba zao ambazo hazijui. Mganga huyo wa jadi ambaye alidai jina lake limesajiliwa pia katika chama cha waganga cha utafiti na magonjwa sugu nchini (CHAMUTA) amekuwa akifanya shughuli zake bila kutoza fedha, hususani kazi ya kusafisha mitaa. ``Hawa hawana hata karatasi ya uhalali wa jina hilo. Halafu mimi situmii utaratibu wa kutoza fedha na huwa nawasiliana na uongozi wa mtaa husika, wakikubali niwafanyie kazi nawataka waniandikie ruhusa hiyo,`` alisema. Alisema iwapo itagundulika ni kweli watu hao walikuwa wakilitumia jina lake `kutapeli` watu atawadai fidia lakini hawezi kuwazuia kufanya kazi zao na kujitafutia umaarufu kupitia majina mengine. Hata hivyo, alikiri kuwa mmoja kati ya vijana waliokamatwa, Rajab Shomari, mkazi wa Kisarawe, alikuwa akifanya naye kazi mwaka mmoja uliopita lakini alimtoroka baada ya kumuibia `tunguli`. Wanaoshikiliwa na Polisi kwa mahojiano ni Tete Diamwana au ``Wakutambatamba``, Mkazi wa Sumbawanga, Sharifu Sharifu mkazi wa Mombo na Rajab Shomari, mkazi wa Chole Kisarawe. Wakihojiwa kituoni hapo, watuhumiwa walikiri kufanya kazi za kiganga katika maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Morogoro lakini wakadai kwamba jina hilo la Manyaunyau walipewa na wakazi kutokana na kunywa damu ya paka. Mmoja wa wakazi wa Mtaa wa CCM Mafiga, Bi. Sikudhani Kassim aliwaambia waandishi wa habari nje ya kituo hicho cha Polisi kuwa watu hao waliokamatwa waliwatapeli kutokana na imani zao potofu za kukubali kuondolewa matatizo ya kishirikina katika maeneo yao. ``Tulijichanga mwenye elfu mbili, tatu na hata zaidi ili tufikishe laki moja waliyokuwa wakitaka lakini tulifikisha 75,000 tu wakakubali, lakini tuliposikia kaja Manyaunyau halisi ikabidi tuje tuthibitishe kama ni kweli au la,`` alisema dada huyo.
SOURCE: Nipashe

0 comments:

 
Design by Kwetu Bongo